Waziri wa Ujenzi Mhe. Abdallah Ulega ametembelea na kukagua maendeleo ya ujenzi wa barabara ya Same–Mkomazi–Ndungu yenye urefu wa kilomita 37 inayojengwa kwa kiwango cha lami wilayani Same, mkoani Kilimanjaro,.
Akizungumza katika ziara hiyo Waziri Ulega alimtaka mkandarasi M/S China Communication Construction Company Ltd. anayetekeleza mradi huo kuongeza kasi ili ukamilike kwa wakati .
Mradi huo unatekelezwa kwa lengo la kuimarisha miundombinu ya usafiri, kurahisisha mawasiliano na kuchochea ukuaji wa shughuli za kiuchumi kwa wananchi wa maeneo hayo.
Waziri Ulega alimuelekeza msimamizi wa mradi huo kuhakikisha wananchi wanaofanya kazi katika mradi huo wanalipwa kwa wakati na kwa viwango vinavyokubalika kisheria hapa nchini.
Sambamba na hilo, Waziri Ulega amemtaka mkandarasi kutoa vyeti vya ushiriki (certificates) kwa vijana wanaoshiriki katika ujenzi wa barabara hiyo ili kuwapa fursa ya kushiriki katika miradi mingine ya maendeleo inayotekelezwa na Serikali.
Kwa upande wake, Mkuu wa Mkoa wa Kilimanjaro, Mhe. Nurdin Babu, amesema kukamilika kwa mradi huo kutakuwa chachu ya maendeleo ya kiuchumi kwa wananchi wa maeneo husika, akibainisha kuwa wakazi wengi wa eneo hilo ni wakulima ambao watanufaika kwa kusafirisha mazao yao kwa urahisi kwenda masokoni.
Hakimiliki©2018 Halmashauri ya Wilaya ya Same.Haki zote zimehifadhiwa.